''Badilisha Maisha yako kwa kumpokea Yesu Kristo kuwa Mwokozi wa Maisha Yako.''

Sunday, March 29, 2020

UTAKATIFU

Mhubiri: Mch. Kiongozi Abdiel M. Mhini
Maandiko : 1Petro 1:13-24, Zaburi 1:1-6, Waebrania 12:14

1Petro 1:14-16 "Kama watoto wa kutii msijifananishe na tamaa zenu za kwanza za ujinga wenu; bali kama yeye aliyewaita alivyo mtakatifu, ninyi nanyi iweni watakatifu katika mwenendo wenu wote; kwa maana imeandikwa, Mtakuwa watakatifu kwa kuwa mimi ni mtakatifu."


Utakatifu ni kuiacha dunia na kumtumikia Mungu wako, mstari wa 15, Mungu anakuita uwe mtakatifu uachane na mwenendo wa mwanzo, mwenendo wa dhambi. Ishi maisha ambayo Mungu anayakubali ambayo ni ya utakatifu. Katika Mstari wa 17 inasema tutembee kwa hofu katika wakati wa kukaa hapa duniani, hapa duniani tunapita nyumbani kwenu ni mbinguni ambapo hatuwezi fika bila huo Utakatifu, Yakupasa uwe mtakatifu.

Chunguza mwenendo wako sasa, unapoingia na kutoka mwenendo wa maisha yako upoje? Rudi kwa Bwana leo. Hapa duniani sisi ni wapitaji hatutakaa siku zote duniani, kwahiyo andaa sehemu unayoenda. Katika mstari wa 23 inasema umezaliwa mara ya pili kwa mbegu isiyoharibika na mbegu hiyo ni Yesu Kristo.

Katika Zaburi 1:1- Mtu mtakatifu amelinganishwa na mti ulio kando kandi ya vijito vya maji ambao haukauki na uzaao kwa majira yake. Ukiona unakaa zaidi kwenye mabaraza ya wenye mizaha ujue Roho Mtakatifu ameondoka. Ukiwa ndani ya Yesu, Unakuwa kiumbe kipya ya kale yamepita. Inapaswa tuwe matakatifu kama Yesu alivyo mtakatifu

Unajitaidi mambo mengi lakini hufanikiwi kwasababu ya sio mtakatifu, wako watu wanafanya dhambi kwa siri sana, maisha ya jinsi hiyo utaaibika siku moja maana Mungu atakuweka wazi adharani kwasababu Mungu yupo kinyume na dhambi, sasa kwanini uaibike kwanini usimrudie Mungu kwa moyo wote. Uovu ulionao huwezi kumficha Mungu, tubu sasa!


Waebrania 12:14 "Tafuteni kwa bidii kuwa na amani na watu wote, na huo utakatifu, ambao hapana mtu atakayemwona Bwana asipokuwa nao;"

Zaburi 24:3-5 "Ni nani atakayepanda katika mlima wa Bwana? Ni nani atakayesimama katika patakatifu pake? Mtu aliye na mikono safi na moyo mweupe, Asiyeiinua nafsi yake kwa ubatili, Wala hakuapa kwa hila. Atapokea baraka kwa Bwana, Na haki kwa Mungu wa wokovu wake."

Hakuna chochote kinyonge kitakachingia mbinguni maisha yako mwenendo wako lazima ubadilike, hebu mrudie Mungu kwa toba, leo hii kama Bwana Yesu akirudi akakukuta  hujatubu kwanini uingie kwenye hasara ya kubaki?, Bwana Yesu anarudi saa yoyote je akirudi utaenda? Je una sifa za kwenda na Yesu Kristo? Tubu sasa..

Sunday, February 2, 2020

MKRISTO WA KWELI

Mhubiri: Mch. Kiongozi Abdiel M. Mhini
Maandiko: Matendo 5:1-11

Mkristo wa kweli ni yule anayeishi maisha matakatifu yanayompendeza Mungu na kuzingatia tunda la Roho. Ni yule anayesoma Neno la Mungu na kuliiishi, ni yule anayedumu katika kuomba.

Matendo 5:1-11
 "1 Lakini mtu mmoja jina lake Anania, pamoja na Safira mkewe, aliuza mali, 2 akazuia kwa siri sehemu ya thamani yake, mkewe naye akijua haya, akaleta fungu moja akaliweka miguuni pa mitume. 3 Petro akasema, Anania, kwa nini Shetani amekujaza moyo wako kumwambia uongo Roho Mtakatifu, na kuzuia kwa siri sehemu ya thamani ya kiwanja? 4 Kilipokuwa kwako, hakikuwa mali yako? Na kilipokuwa kimekwisha kuuzwa, thamani yake haikuwa katika uwezo wako? Ilikuwaje hata ukaweka neno hili moyoni mwako? Hukumwambia uongo mwanadamu, bali Mungu. 5 Anania aliposikia maneno haya akaanguka, akafa. Hofu nyingi ikawapata watu wote walioyasikia haya. 6 Vijana wakaondoka, wakamtia katika sanda, wakamchukua nje, wakamzika. 7 Hata muda wa saa tatu baadaye mkewe akaingia, naye hana habari ya hayo yaliyotokea.8 Petro akamjibu, Niambie, Mlikiuza kiwanja kwa thamani hiyo? Akasema, Ndiyo, kwa thamani hiyo. 9 Petro akamwambia, Imekuwaje hata mkapatana kumjaribu Roho wa Bwana? Angalia, miguu yao waliomzika mumeo ipo mlangoni, nao watakuchukua nje wewe nawe. 10 Mara akaanguka miguuni pake akafa; wale vijana wakaingia wakamkuta amekufa, wakamchukua nje, wakamzika pamoja na mumewe."


Anania na mke wake Safira walipanga kumdanganya Roho Mtakatifu lakini Mungu hadanganyiki, Mungu anatisha akawaua hapo hapo. Amua Leo kuwa mkristo wa Kweli, hii ni January amua kupanga kusoma Biblia kwa mpangilio kama kwa sura, amua kuwa na mpango mzuri wa maombi, amua kuongeza viwango vyako kwa kumpenda Mungu, uzembe ulioufanya mwaka jana katika kumpenda Mungu usiurudie na mwaka huu. Dumu katika uaminifu ukimpenda Mungu siku zote.

Tuesday, January 28, 2020

KIU YA KWELI ILETAYO MABADILIKO

Mhubiri: Mrs. Lucy Masembo
Maandiko: Yohana 4:1-26

Yohana 4:7-15
7 Akaja mwanamke Msamaria kuteka maji. Yesu akamwambia, Nipe maji ninywe 8 Kwa maana wanafunzi wake wamekwenda mjini kununua chakula. 9 Basi yule mwanamke Msamaria akamwambia, Imekuwaje wewe Myahudi kutaka maji kwangu, nami ni mwanamke Msamaria? (Maana Wayahudi hawachangamani na Wasamaria.) 10 Yesu akajibu, akamwambia, Kama ungaliijua karama ya Mungu, naye ni nani akuambiaye, Nipe maji ninywe, ungalimwomba yeye, naye angalikupa maji yaliyo hai. 11 Yule mwanamke akamwambia, Bwana, huna kitu cha kutekea, na kisima ni kirefu; basi umeyapata wapi hayo maji yaliyo hai? 12 Je! Wewe u mkubwa kuliko baba yetu, Yakobo, aliyetupa kisima hiki, naye mwenyewe akanywa maji yake, na wanawe pia, na wanyama wake? 13 Yesu akajibu, akamwambia, Kila anywaye maji haya ataona kiu tena; 14 walakini ye yote atakayekunywa maji yale nitakayompa mimi hataona kiu milele; bali yale maji nitakayompa yatakuwa ndani yake chemchemi ya maji, yakibubujikia uzima wa milele. 15 Yule mwanamke akamwambia, Bwana, unipe maji hayo, nisione kiu, wala nisije hapa kuteka.


Kiu ni shauku kubwa ya ndani ambayo mtu hawezi kutulia mpaka kile kitu kitimilike. Mwanamke Msamaria alikuwa na kiu ya kumjua Mungu zaidi na zaidi, Kiu ile ilimfanya ampokee Yesu, ilimfanya apate mabadiliko makubwa na baada ya hapo akawa kiumbe kipya, akaanza kuwa muinjilisti akaenda kuwaambia mji wote kuhusu Yesu.

Kiu au shauku ya kumjua Yesu inaleta mabadiliko. Shauku ndani mwako ya kumjua Yesu zaidi na zaidi itakuletea mabadiliko. Yesu Kristo akiingia rohoni mwako maisha yako hayawezi kubaki vile vile ni lazima yatakuwa na mabadiliko, kwa mfano utapata uwezo wa kushinda dhambi. Jawa na shauku ya kumjua Yesu zaidi na zaidi hutabaki kama ulivyo.

Kwanini sasa uwe na Kiu/ Shauku? Kwasababu
1. Kiu itakupa nguvu nyingine ya kutumika kwa ajili ya Mungu, ukikutana na nguvu ya Mungu utapata nguvu mpya ya kumtumikia. Kiu itakupa bidii ya kutumika kwajili ya Mungu.
2. Kiu italeta kutokujihurumia, ukijua Mungu aliyekuita ndani utafanya tu kazi yake.
3. Kiu itafanya kutokuogopa vizuizi  ambavyo vinaweza kutokea
4. Ukiwa na kiu hii inakupa shauku ya kumchagua Yesu kwanza, utaona Yesu kwanza na ndio mambo mengine.

Sunday, December 1, 2019

SIKU YA KUWAPONGEZA WACHUNGAJI

Mhuburi: Mr. Godfrey Zayumba
Maandiko: Warumi 10:12-15

Kuwapongeza wachungaji/ watumishi wa Mungu ni kitu cha maana sana kwasababu wanajitaabisha usiku na mchana kwa ajili yetu, wameacha vyote wamekuja kufanya kazi ya Mungu. Katika wana wa Israeli, watumishi wa Mungu walitokea kwenye kabila la Lawi, na kabila hili halikupewa eneo kama uridhi kwasababu wao maisha yao yalikuwa ni nyumbani kwa Bwana, ndivyo ilivyo hata leo, wachungaji hawafanyi kazi nyingine za kuajiriwa za kuingiza vipato, kwahiyo ni wajibu wetu kuwajali. Wachungaji wanafanya kazi kubwa sana, wewe unapata mafanikio katika kazi yako au biashara  zako ni kwasababu wachungaji wamekuombea, wachungaji wanakuombea mchana na usiku. Kuongoza kanisa lenye watu tofauti na wenye mitazamo tofauti si kazi ndogo bali ni kazi kubwa, wachungaji wanasuluhisha kesi nyingi, ni lazima tutambue kazi yao wanayoifanya na kuwapongeza.

Mambo muhimu ya kuyatambua kuhusu Mchungaji
1. Tuwatambue watumishi wa Mungu; ni lazima tutambue uwepo wao na kuuheshimu, lakini pia tutambue kazi kubwa wanayoifanya.
2. Wanatusimamia
3. Wanatuonya kwa Upendo kwasababu hawataki tuangamie wala umuache Yesu Kristo
4. Kuwastahi sana katika upendo- kumfichia aibu,tuwafichie aibu machungaji wetu, Haruni na Miriam walimsema Mussa gafla miriam akapata ukoma!
5. Kuwakumbuka, ni lazima uwakumbuke mchungaji wako kwenye maombi yako.
6. Wanatuongoza ili twende kwa usahihi
7. Wanatuambia Neno la Bwana, kila siku wanaanda chakula/Neno la Mungu ili upate malisho yaliyo bora 
8. Kuuwatii kwenye kile ambacho wanatuongoza
9. Kuwanyenyekea

Monday, November 25, 2019

KUWA MKRISTO WA KWELI

Mhubiri: Mch. Kiongiozi Abdiel M. Mhini
Maandiko: Luka 14:25-33, 1Petro 2:20-24

Kuwa Mkristo wa Kweli ni kumfuata Kristo kwa vitendo, kuishi kama Kristo alivyoishi, Yesu Kristo alivyokuwa hapa duniani aliishi maisha matakatifu ya hakutenda haki. Ndugu yangu kumfuata Yesu Kristo ni lazima uwe tayari kulipa gharama, kumfuata Yesu ni lazima uwe tayari kupambana na shetani na changamoto zote zitakazokuja mbele yako. Tangu siku unapookoka unakuwa umetangaza vita na shetani. 

Katika Neno tulilosoma, Biblia haisemi uwachukie wazazi wako lakini imemaanisha wazazi au ndugu zako wasiwe kizuizi cha wewe kuacha kumpenda Yeye, hata kama wote wakakutenga Yesu kristo atakusaidia na kukutunza. Utayari wa kuanza yote kwa ajili ya Yesu, hata kama kazi inaingiza pesa nyingi ikiwa inamuuzi Yesu achana nayo, afadhali ukose hiyo hela isiyo na haki ukamfuata Yesu. Kuishi maisha ya Kikristo ni kumfanya Yesu Kristo awe namba moja kwako, achana na vitu vyote vinavyozuia uhusiano wako na Mungu. 

Ndio labda umeshampokea Yesu lakini Je mpaka sasa umekuwa mKristo wa kweli, maisha yako yamefanana na Kristo? Je unamsikiliza Roho Mtakatifu?, Kuwa mkristo wa kweli ni kusikia Roho Mtakatifu na kufanya anayokuongoza hata kama halitawafurahisha watu wanaokuzungu ilimradi ni cha haki na ni mapenzi ya Mungu inabidi ukifanye. 

Lazima uwe mvumilivu, kama kweli unataka uwe mwanafunzi wa Yesu ni lazima ujikane mwenyewe kuna baadhi ya vitu kwasababu umeokoka hutatakiwa kuvifanya.

Matatizo ya kifamilia yasikuzuie kuwa Mkristo wa kweli, Luka 14:26. Mali za hapa duniani hazitakiwi kukuzuia kumfuata Yesu, Mathayo 19:20-24. Ubarikiwe!

Sunday, November 17, 2019

YESU KRISTO BADO ANATENDA HATA SASA

Maandiko: Waebrania 13:8 

Waebrania 13:8
"Yesu Kristo ni yeye yule, jana na leo na hata milele."

Yesu Kristo yu Hai, bado anaishi bado anatenda miujiza bado anaweza kutenda mambo yaliyoshindikana kwa wanadamu. Mungu ni Yule Yule jana leo na hata milele, Yeye habadiliki, hazimii wala hachoki, aliyegawanya bahari ya shamu wana wa Israeli wakapita na kuua jeshi la farao ndiye Mungu hata leo, haijalishi unapitia hali ngumu kiasi gani, Mungu atakutoa kwenye hali hiyo, Yesu Kristo yupo kukusaidia. Yesu alisema katika Mathayo 11:28 "Njoni kwangu, ninyi nyote msumbukao na wenye kulemewa na mizigo, nami nitawapumzisha."

Haijalishi umeteseka kwa kiasi gani, njoo kwa Yesu atakupumzisha, hali ngumu unayopitia mwambie Yesu leo yuko tayari kukusaidia. Yeremia 32:27 "Tazama, mimi ni Bwana, Mungu wa wote wenye mwili; je! Kuna neno gumu lo lote nisiloliweza?" Je kuna jambo gumu la kumshinda Yesu Kristo? jibu ni Hakuna! kwahiyo ile shida yako kubwa kwako mwambie Yesu Kristo na umwamini naye atafanya!

Mathayo 7:7-8 "Ombeni, nanyi mtapewa; tafuteni, nanyi mtaona; bisheni, nanyi mtafunguliwa; Kwa maana kila aombaye hupokea; naye atafutaye huona; naye abishaye atafunguliwa." Yesu Kristo anasema uombe nawe utapewa, mwambie Mungu mahitaji yako. Pia katika Hesabu 23:19 "Mungu si mtu, aseme uongo; Wala si mwanadamu, ajute; Iwapo amesema, hatalitenda? Iwapo amenena, hatalifikiliza?" Mungu ni Mungu sio kama mwanadamu anayetoa ahadi na kubadilika badae, Mungu hasemi uongo ahadi zake zote alizokuahidi zitatokea, amesema ukiomba utapata basi omba na uamini kwamba utapokea na kweli itatokea. Mungu akubariki sana.


Sunday, October 27, 2019

UTENDAJI WA MUNGU NYUMA YA MAMBO UNAYOPITIA (WORK OF GOD BEHIND THE SCENE)

Mhubiri: Mch. Isack Challo
Maandiko: Mwanzo 45:1-8, Mwanzo 15:12-16

Mwanzo 45:1-8
"Hapo Yusufu hakuweza kujizuia mbele yao wote waliosimama karibu naye. Akapiga kelele, na kusema, Mwondoeni kila mtu mbele yangu. Wala hakusimama mtu pamoja naye, Yusufu alipojitambulisha kwa nduguze. Akapaza sauti yake akalia, nao Wamisri wakasikia. Watu wa nyumba ya Farao nao wakasikia. Yusufu akawaambia ndugu zake, Mimi ndimi Yusufu; baba yangu angali hai bado? Wala ndugu zake hawakuweza kumjibu, maana waliingiwa na hofu mbele yake. Yusufu akawaambia ndugu zake, Karibuni kwangu; basi, wakakaribia. Akasema, Mimi ni Yusufu, ndugu yenu, ambaye mliniuza kwenda Misri. Basi sasa, msihuzunike, wala msiudhike nafsi zenu, kwa kuniuza huku; maana Mungu alinipeleka mbele yenu kuhifadhi maisha ya watu. Maana miaka hii miwili njaa imekuwa katika nchi, na iko tena miaka mitano isiyo na kulima wala kuvuna. Mungu alinipeleka mbele yenu kuwahifadhia masazo katika nchi, na kuwaokoa ninyi kwa wokovu mkuu. Basi si ninyi mlionipeleka huku, ila Mungu; naye ameniweka kama baba kwa Farao, na bwana katika nyumba yake yote, na mtawala katika nchi yote ya Misri".


Huu ni moja ya ushuhuda mzuri sana wa jinsi Mungu anavyofanya kazi kwa njia ya tofauti mno zaidi ya vile tunavyodhani. Yusufu alivyokuwa mdogo aliota ndoto kwamba familia yao yaani baba na ndugu zake watamuinamia yeye na wakati yeye ndiye mtoto wa mwisho, na ndoto zile ziliendelea kaka zake wakata kumuua ili asiwasumbue na zile ndoto zake. Kwahiyo kaka za Yusufu walitaka kuiua ile ndoto wasijue kwamba Mungu anafanya kazi nyuma ya mambo unayopitia, wakamuuza kama mtumwa kwa wamisri wakizani kuwa watakuwa wamezuia ile ndoto, wasijue kwamba kwa kufanya vile wametengeneza daraja kwa Yusufu kwenda kwenye hatua nyingine zaidi.

Yawezekana na wewe leo unapitia hali ngumu unajiuliza kwanini mambo yanakuwa hivyo, kumbe kupitia shida hiyo ni daraja la kwenda hatua nyingine, maadai zako wanaweza wakadhani wamekumaliza kumbe wamekuwa ni sababu ya wewe kwenda hatua nyingine ya mafanikio yako.

Ukisoma Zab 105:7-19, utaona kwamba Yusufu alienda Misri akiwa amefungwa minyororo kama mtumwa akiwa katika maumivu hakujua nini kitatokea, lakini kumbe Mungu alikuwa anafanya kazi nyuma ya pazia, kumbe Mungu alikuwa naye hakumuacha. Katika hali ngumu muda mwingine ni vigumu kuamini kwamba Mungu bado yupo pamoja na wewe. Yusufu alienda Misri akiwa ni mtumwa mwenye maumivu kumbe ilikuwa ni mpango wa Mungu ili Neno lake litimie ili ile ndoto aliyoiota itimie.

Mipango ya Mungu katika maisha yako itatimia tu haijalishi watajitahidi kiasi gani kuzuia mafanikio yako, wakati wa Mungu ukifika kila kitanyamaza hakitaweza kuzuia kamwe. Kama una ombi ambalo bado Mungu hajalitenda, usikate tamaa, na umtegemee sana Roho Mtakatifu. Wakati wa Mungu ukifika! Umefika! hakuna atakayeweza kuzuia.