''Badilisha Maisha yako kwa kumpokea Yesu Kristo kuwa Mwokozi wa Maisha Yako.''

Monday, April 8, 2013


NAMNA YA KUMSIFU NA
KUMWABUDU  MUNGU
-------------------------------------------------------------------------------------

Tumejifunza mambo mengi sana yaliyokuhamasisha na yaliyokupiga deni uwe kiumbe wa kumsifu na kumtukuza Mungu. Tunapomsifu mtu, huwa tunaelezea yale ambayo yanamtofautisha na wengine. Hivyo basi, ufikapo katika muda wa kumsifu na kumwabudu Mungu, ujue namna ya kuifanya sifa yako na ibada yako kwa usahihi.
                   Na ili kumpa Mungu sifa na ibada, ni lazima na ni muhimu sana ujue mambo ambayo yanamstahilisha Mungu wetu kusifiwa na kutukuzwa. Kwa kutumia sifa na tabia za Mungu, utaweza kumsifu na kumwabudu vizuri. Hakuna kiumbe kingine chochote kinazo zile sifa kuu tano za Mungu, isipokuwa yeye Mungu Jehova peke yake.
                    Kwahiyo, na hizo ndizo zinayomstahilisha yeye kusifiwa na viumbe wake. Katika sura ya nane, tumeshajifunza mambo yanayomstahilisha Mungu kupewa sifa. Kwakuwa sasa unayajua, basi tumia mambo hayo uendapo mbele za Mungu katika katika ibada yako ili kumsifu na kumwabudu. Unapomueleza Mungu sifa zake na tabia zake (vile alivyo) hapo unakuwa unamsifu na kumwabudu.

Tofauti ya kusifu na kuabudu
Naomba urudie kuisoma sura ya kwanza ya kitabu hiki, ambapo nimefundisha vizuri maana ya kumshukuru Mungu, kumsifu Mungu na kumwabudu Mungu. Hii itakusaidia kutofautisha mambo haya kwa nia ya kuyaelewa au kuyaelezea kwa mtu mwingine. Nilisema hivi,
Ibaba ni kitendo cha mtu kumtukuza, kumhimidi, kumwinua, kumwadhimisha, kumshukuru na kumheshimu Mungu kwa vile alivyo na kwa yale aliyoyatenda. (Appreciation and admiration for who God is and for what He has done). Lakini haya mambo matatu, yanayofanana sana na si rahisi sana kuyatenganisha kimaelezo au kivitendo.
                Lakini tuendapo mbele za Mungu kwa ibada, iwe ni chumbani kwako au sebuleni kwako au kwenye gari lako au kanisani kwako, kusifu na kuabudu na kushukuru, ni mambo yanayofanyika kwa kuingliana sana. Sio sheria kwamba, hautakiwi kuchanganya sifa na kuabudu na kushukuru, hapana. Hebu soma tena sura ya kwanza vizuri. Kati ya mengi, nilisema hivi;
                Haya mambo matatu, kusifu, kushukuru na kuabudu, ni mambo yanayofanana sana. Inaweza ikawa vigumu kidogo kuyatenganisha kimaelezo au kivitendo. Ni ngumu kidogo, kufanya kimoja pasipo wenzake, kwasababu ni mambo yanayokwenda kwa pamoja sana. Lakini kwa tafsiri zake, yako hivi;
1.    Kumshukuru Mungu;- Ni ile hali ya kumueleza Mungu jinsi tunavyothamini (Appreciate and Admire) wema wake, fadhili zake na baraka zake katika maisha yetu.

2.    Kumsifu Mungu; - Ni kumueleza Mungu juu ya matendo yake makuu na ya ajabu aliyoyafanya. Au ni kuwaeleza wengine kuhusu matendo makuu ya Mungu aliyoyafanya katika maisha yetu au kwa watu wengine.

3.    Kumwabudu Mungu; - Ni kumueleza Mungu tukuzo zetu, heshima yetu na upendo wetu kwake kwasababu ya uzuri wa tabia zake kwetu. (Credentials and Characters). 
Kwahiyo, tuendapo mbele za Mungu kwa ibada, iwe ni chumbani kwako au sebuleni kwako au kwenye gari lako au kanisani kwako, ili kumsifu na kumwabudu na kumshukuru Mungu, uwe huru kujimimina mbele za Mungu kwa kufanya vyote vitatu, kwa namna moyo wako utakavyokuwa unaongozwa na Roho Mtakatifu. Vyote vitatu vinatengeneza ibada takatifu kwa Mungu.
                Katika sura inayokuja, nimefundisha vizuri namna ya kuingia katika ibada na hata kupenya na kufika katika chumba cha ndani kabisa cha uwepo na utukufu wa Mungu; ili unapokwenda mbele za Mungu wetu, uweze kukutana na nguvu zake katika utukufu wake.
                 Lakini hapa chini nimeziweka kwa ufupi ili kukukumbusha. Na pia nimekuongezea na mambo mengine yanayotakiwa katika kumsifu na kumtukuza Mungu. Kwahiyo, utengapo muda wa kukaa mbele za Mungu wetu kwa ibada, msifu na kumtukuza Mungu kwa mambo yafuatayo,

1.    Mtukuze Mungu kwa Sifa zake za Uungu (ambazo hakuna mwingine aliye nazo) Kwamba;
a)    Jehova ni Mungu wa Milele
b)    Jehova ni Mungu Mtakatifu
c)    Jehova ni Mungu Aliye kila mahali
d)    Jehova ni Mungu Anayejua mambo yote
e)    Jehova ni Mungu Aliye na nguvu zote na  
      anaweza kufanya mambo yote kabisa.

Nimezielezea vizuri hizi sifa za Uungu, katika sura ya kwanza. Hizi ni baadhi tu ya sifa za Mungu, sio zote. Kwa hivyo basi, pamoja na namna nyingine ambazo utajifunza kumsifu na kumwabudu Mungu, hebu uwe unamsifu Mungu kwa mambo haya au kwa sifa zake hizi pia.

Msifu Mungu kwa;
2.    Kwasababu ya Tabia zake
3.    Kwasababu ya Matendo yake ya Ajabu
4.    Kwasababu ya Fadhili nyingi na kuu mno
5.    Kwasababu ya Ahadi zake kubwa za thamani

2.   Mtukuze Mungu  kwa Tabia zake
Neno la Mungu, linatuonyesha jinsi ambavyo Mungu wetu ana tabia na kawaida nyingi nzuri ambazo kwa hizo, tunavutiwa na tunapigwa deni kumsifu na kumwabudu. Kwa mfano ; Biblia inasema kwamba, Mungu wetu amejaa Upendo, usio na mwisho. Ni Mwingi wa huruma, Si mwepesi wa hasira, sifa yake ni kuwa na rehema daima. Soma mistari ifuatayo, ili uone zaidi. Lakini kwasababu ya sifa hizi (Tabia zake), tunapigwa deni kumsifu na kumwabudu. *Zaburi 103:8, Kutoka 34 :6,
*Efeso 3 :18-19, Daniel 9 :4, Ufunuo 19 :11

3.     Mtukuze Mungu  kwa Matendo yake ya ajabu.
Mungu wetu ni Mungu aliyefanya mambo ambayo hakuna tena, awezaye kufanya. Kwa mfano; ndiye aliyeziumba na kuzitundika sayari zote za ulimwengu huu, bila minyororo wala nguzo. Mungu wetu ndiye anayesababisha mioyo yetu inadunda, bile kuwekewa betrii wala chaji (charge). Au ni lini ulichomeka moyo wako katika soketi ya umeme kama unavyochomeka simu yako ili kupata umeme?
        Nina uhakika, hakuna mtu anayefanya hivyo. Sasa unadhani moyo wako unadundaje? Hizo ni kazi za ajabu za Mungu wetu.na hakuna mtu awezaye kuzifanya. Kwasababu ya matendo yake ya ajabu, Mungu wetu anastahili kusifiwa na kutukuzwa. Soma mistari ifuatayo kwa umakini. Utaweza kuona kwa uchache, jinsi maandiko yanavyoeleza juu ya matendo makuu ya Mungu.
Haya ni maelezo ya watu wa Mungu ambao kwa kumjua Mungu, waliweza kueleza ukuu wake vizuri, ili na sisi tunaosoma maandiko yao, tunajifunza juu ya ukuu wa Mungu, uweza wa Mungu na tabia za Mungu wetu. Soma vizuri Kitabu cha Daniel 6:25-27,  Nehemia 9:6,  Zaburi 147:1-18,  na Zaburi sura ya 136:4-26

4. Mtukuze Mungu  kwa Fadhili zake.
Mungu wetu ni Mungu atupaye baraka na fadhili nyingi kila siku. Fikiri wema ambao Mungu amekufanyia maishani mwako, na hata katika siku ya leo tu. Kuna vingi ametupa ambavyo wengi walitamani, lakini hawakupewa. Uhai, afya, ulinzi, rehema, chakula, fedha, shule, simu, gari, nyumba, ajira, mke, mume, watoto, na hata wazazi.
                  Sio kila mtu bado ana wazazi. Na wengine wamezaliwa hawajawahi kuwajua wazazi wao. Kwakweli fadhili na baraka za Mungu ni nyingi sana; ukiamua kuziorodhesha, utakesha. Sasa, kwa fadhili zote hizi alizotujalia, basi Mungu wetu anstahili kusifiwa.
*Zaburi 103:1-5,  Zaburi 107:21,  2Nyakati 20:21

5.    Mtukuze Mungu  kwa Ahadi zake.
Ni Mungu aliyetuahidi watu wake, mambo mengi sana mazuri. Ametupa ahadi kubwa mno na za thamani sana. Ni ahadi za kutupa baraka, heshima na utajiri. Kwa ahadi hizi pia, anastahili kusifiwa * 2Petro 1:3-4,  Efeso 1:3-4,  Kumbu 4:4-8
                Kwa ufupi, hivi ndivyo unavyotakiwa kumsifu na kumwabudu Mungu. Kadri unavyoanza kufanya hivi kwa vitendo, utaendelea kujifunza kufanya huduma hii ipasavyo, nawe utajikuta unakutana na nguvu za Mungu kwa namna ya tofauti maishani mwako.

MSIFU MUNGU KWA MAJINA YAKE.
Majina ya Mungu, hueleza sifa za Mungu, Tabia za Mungu au Matendo ya Mungu. Mfano; Wayahudi wanamwita Mungu El-Shaddai. Ni neno lenye majina mawili ndani yake. El’  maana yake Mungu, na ‘Shaddai’ lenye maana itokanayo na neno ‘Shad’ yaani Titi (Ziwa) la mama anyonyeshaye.
        Kutokana na ukweli kwamba, titi/ziwa la mama anyonyeshaye, linampa mtoto mchanga kila kitu anchohitaji. Maziwa ya mama yake, humpa mtoto kila kitu mtoto anachohitaji. Ndani ya maziwa kuna vitamini, protini, wanga, mafuta, madini, maji, na kila kitu mtoto anachohitaji. Maziwa ya mama, yanamtosheleza mtoto kwa kila kitu. Hivyo, Waisraeli wanapomwita Mungu El-Shaddai, wanamaanisha kuwa, kama ziwa linavyo mtosheleza mtoto, vivyo hivyo, Mungu ni ‘Mtoshelezi’ kwetu. Halleluyah!
       Hivyo, kila jina la Mungu, linabeba aidha Sifa yake au Tabia yake au Matendo yake. Ndio maana Mfalme Daudi anasema

“Mpeni Bwana, enyi wana wa Mungu … Mpeni Bwana utukufu kwa jina lake. Mwabuduni Bwana kwa uzuri wa utakatifu.” (Zab 29:1-2) Msifuni Bwana kwa kuwa Bwana ni mwema, Liimbieni Jina lake, kwakuwa lapendeza.(Zaburi 135:3).

Na Bwana Yesu alitufundisha kuanza sala namna hii;

Baba yetu uliye mbinguni, jina lako tukutuzwe, hakafu Ufalme wako uje hapa duniani.




Kwahiyo, unaweza pia kumsifu Bwana kwa majina yake. Majina ya Mungu, hueleza aidha sifa za Mungu au tabia za Mungu au Matendo makuu ya Mungu. Yafuatayo hapa chini, ni baadhi ya majina ya Mungu kwa lugha ya Kiebrania, yatakayokusaidia kumsifu, kumwabudu na kumshukuru Mungu.
MAJINA YA MUNGU

Jina la Mungu                           Maana yake                          Mstari wa Biblia        
1.             Adonai -                       Mungu Mwenye enzi yote - Mwa 15:2-8, Kut 6:2-3
2.             El-Ohim -                     Mungu Muumbaji        -  Mwa 33:20, Kol 1:16-17
3.             El-Elyon -                     Mungu Aliye juu zaidi       -   Mwa14:18, Dan 4:34
4.             El-Gibbor       -            Mungu Mwenye Nguvu    -           Isa 9:6,  Zab 147:5
5.             El-Hai -                        Mungu Aliye Hai/Anaishi   -  Josh 3:10,  1Sam17:26
6.             El-Olam -                     Mungu wa Milele                               -  Ufu 4:8,  Kut 3:14
7.             El-Roi -                       Mungu Aonaye kila kitu                - Mith 15:3, Zab 32:8
8.             El-Shaddai -                Mungu Mtoshelezi     -  Mdo 17:28, Kumb 8:4
9.             Jehovah -                  Ajitegemeaye kuwepo -Kut 6:2-8,  Mdo 17:24-25
10.           Jehovah Shalom    -Mungu Amani yetu           - Amu 6:22-24
11.           Jehovah Rapha   -    Mungu Atuponyaye                -  Kut 15:26
12.           Jehovah Jireh   -       Mungu Mtoaji wetu           - Mwa 22: 8, 14
13.           Jehovah Nissi  -       Mungu Ushindi wetu           - Kut 14:13-14
14.           Jehovah Saboath  -  Bwana wa Majeshi             -  Malaki 3:7
15.           Jehovah Shammah -  Bwana ni Aliyepo                     -  Kut 3:14
16.           Jehovah Rohi           -  Bwana  ni Mchungaji wangu   -  Zab 23:1
17.           Jehovah Tsidkenu  -  Bwana ni Haki yetu              -  Yer 23:6
18.           Jehovah Mekaddishem  -  Bwana Atutakasaye  -  Kut 31:13



Namna  za  kumshukuru, kumsifu,  na  kumwabudu Mungu  wetu.

Kwahiyo, katika maisha yetu sisi, kama waumini, tunatakiwa kumpa Mungu wetu ibada, (kumshukuru, kumsifu na kumwabudu) kwasababu ya mambo yote hayo niliyoyataja. Tunatakiwa kumtukuza Mungu kwasababu ya sifa zake, na kwasababu ya tabia zake, na matendo yake na fadhili zake na ahadi zake kwetu.
      Sasa basi, hapa chini, nimekuwekea njia kuu tatu ambazo unaweza kumsifu na kumtukuza Mungu kwazo. Utengapo muda wa kwenda mbele za Mungu, unaweza kutuia njiia kuu zifuatazo; Kumtukuza Mungu kwa,

  1. Kumwimbia nyimbo za kumsifu na kuwabudu
  2. Kumweleza au kusimulia kwa maneno
  3. Kumtolea Mungu sadaka na dhabihu




 Wako katika kazi ya Mungu

Mwl. Mgisa Mtebe

No comments:

Post a Comment