''Badilisha Maisha yako kwa kumpokea Yesu Kristo kuwa Mwokozi wa Maisha Yako.''

Sunday, July 8, 2018

ISHI KWA KUFUATA MAAGIZO YA MUNGU

Mhubiri: Mch. Kiongozi Abdiel M. Mhini
Maandiko: 1Petro 1:13-25

Kuishi kwa kufuata maagizo ya Mungu, ni kuishi kwendana na mapenzi ya Mungu. Ili uishi kwendana na mapenzi ya Mungu ni lazima uwe unajitakasa maisha yako kila mara. Ili uishi maisha ya kumpendeza Mungu ni lazima uache kufuata mambo ya dunia hii. Umeamua kuwa na Yesu basi ishi kwa kufuata yale Yesu anayokuelekeza bila mchanganyo wa Yesu kidogo na mambo ya duniani, Yesu atakutapika. 

Katika Neno la leo, Petro anaeleza vizuri sana kuwa, kabla ya kumfuata Yesu yaani kabla ya kuokoka unaishi maisha ya mchanganyo, maisha yasiyompendeza Mungu kwasababu ya ujinga wa kutokujua Kweli ya Mungu, lakini sasa baada ya kumpokea Yesu hatutakiwi tena kuenenda kama zamani bali tunatakiwa kuishi maisha ya kujitakasa, maisha ya kufuata maagizo ya Mungu, maisha ya utakatifu.  

Ili uweze kuishi kwendana na mapenzi ya Mungu ni lazima uwe unasoma Biblia na uwe na muda wa kuomba. Kama ilivyo mafanikio yoyote huwa hayatokei hivi hivi tu mpaka uweke bidii fulani vivyo hivyo ili ufanikiwe kuishi maisha matakatifu ni lazima uwe na bidii ya kusoma Neno, kulitafakari na kuomba. Watu wengi sasa wako tayari kukesha kwa bidii kuangalia 'World Cup' lakini hawako tayari kukesha kuomba. Ni lazima uwe na bidii ya kumpenda Mungu bila hivyo mambo ya dunia yatakuvuta. Ni lazima ukubali kuacha kabisa maisha ya michanganyo ndipo utakapo fanikiwa sana.

No comments:

Post a Comment