''Badilisha Maisha yako kwa kumpokea Yesu Kristo kuwa Mwokozi wa Maisha Yako.''

Sunday, July 15, 2018

MUNGU HUMTUNZA MTU WAKE MWAMINIFU

Mhubiri: Mr. Frank Mwalongo
Maandiko: Danieli 1:1-21 

Mfalme Nebukadreza wa Babeli, aliteka Yerusalemu kwahiyo akawa na nguvu ya kuchukua watumwa. Akaamuru wachukuliwe vijana waliotokea kwenye familia za kifalme na walio na sifa nzuri, watunzwe vizuri na kufundishwa kwa miaka mitatu kwa ajili ya kufanya kazi katika nyuma ya mfalme. Kwahiyo wakapewa chakula maalum kitokacho nyumbani kwa mfalme ili wawe na afya njema. Lakini Danieli na wenzake walivyoona kile chakula kina unajisi ndani yake, kwa uaminifu waliokuwa nao mbele za Mungu wakaazimia moyoni mwao kutokula chakula kile wala kunywa divai. Wakaamua kulinda uhusiano wao na Mungu.

Unapokuwa mwaminifu kwa Mungu, Mungu anakutetea. Danieli na wenzake wakaaomba wapewe mtama na maji tu, Mungu akawafanya wanawiri wenye afya bora kuliko vijana wengine waliokuwa wanakula chakula cha mfalme. 

Danieli na wenzake walikuwa tayari kula mtama na maji kwa miaka mitatu (3) kwaajili Tu ya kulinda uhusiano wao na Mungu. Je, wewe uko tayari kiasi gani kulinda uhusiano wako na Mungu? Uko tayari kiasi gani kuacha vitu au mambo yanayoonekana ni mazuri kwa ajili ya Mungu? Je uko tayari kuacha rushwa ya pesa kubwa kwajili ya kulinda uhusiano na Mungu wako, au utasema ngoja nilifanye hili halafu nitatubu. Hata siku moja usikubali kutokuwa mwaminifu mbele za Mungu wako maana kuna faida kubwa sana.

Baada ya ile miaka mitatu, Danieli na wenzake wakaonekana bora sana mbele ya mfalme kuliko vijana wengine wote, na wenye hekima sana mara kumi (10) zaidi ya waganga wa Babeli. 

Unapomtumikia Mungu, Mungu atakutunza wala hupotezi hata kidogo, Mungu atakujali mno. Hakuna hasara ya kumtumikia Mungu bali faida ndio zipo nyingi sana. Hebu amua leo, azimia moyoni mwako kuwa mwaminifu kwa Mungu wako. Mtumikie sana Mungu kwa uaminifu wote wala hutapoteza kitu, Mungu anatunza watu wake. Hakuna aliyemtumikia Mungu kwa uaminifu akajuta! Unapomtumikia Mungu kwa uaminifu Mungu anakubariki kila sehemu ya maisha yako. Jitenge na kila uovu linda sana utakatifu wako. Ubarikiwe

No comments:

Post a Comment