''Badilisha Maisha yako kwa kumpokea Yesu Kristo kuwa Mwokozi wa Maisha Yako.''

Sunday, August 27, 2017

NYUMBA YA YAIRO KUTEMBELEWA NA YESU

Mhubiri: Mch. Kiongizi, Abdiel M. Mhini
Maandiko: Marko 5:21-24,35-43

Yairo alikuwa ni kiongozi wa sinagogi lakini na hayo yote alikuwa ana shida hakuweza kumponya mtoto wake. Aliposikia habari za Yesu kwamba anaponya anatenda miujiza, akaamua kuchukua hatua ya kwenda kumtafuta Yesu, kwahiyo alifunga safari mpaka kwa Yesu kwasababu haikuwa karibu ili kumuomba aje nyumbani alipo binti yake anayeumwa. Lakini watu wakamtaarifu kuwa asimsumbue mwalimu kwasababu binti yake ameshakufa, hapo hapo Yesu akamwambia asiogope bali aamini tu. 

Kuna wakati mwingine unapoendelea kumuomba Mungu unaona mambo yanazidi kuharibika au watu wanazidi kukukatisha tamaa, lakini leo Yesu anakutia moyo kwamba usiogope bali amini tu, muujiza wako bado upo, Ibrahimu na Sara walimwamini Mungu kwa miaka mingi kwamba atatimiza ahadi ya mtoto na badae walipokea muujiza wao. Hapa tunajifunza kuhusu imani, usiogope, mahitaji yanakuja kwa aina tofauti tofauti lakini yote Yesu anayo majibu yake. 

Yesu alipofika nyumbani mwa Yairo watu walikuwa wanalia lakini Yesu akawauliza kwanini mnalia? mtoto hajafa bali amelala lakini wakamcheka na kuona huyu ni mtu wa aina gani. lakini Yesu alipomshika mkono mtoto yule na kumwambia msichana inuka! na mtoto yule akaamka, hapo ndipo walipoelewa uweza wa Yesu kwa muujiza mkubwa sana. 

Yesu anatenda miujiza hata sasa! na ataendelea kutenda, yawezekana leo wakati huu unahitaji lako na unahitaji muujiza, Yesu yuko tayari kukutembelea kama alivyomtembelea Yairo kama tu utamhitaji na kumkaribisha ndani mwako. Yairo aliombwa kutembelewa na Yesu na wewe leo mkaribishe Yesu akutembelee. Ufunuo 3:20 Yesu anapiga hodi, ukimfungulia atakuja kwako na kuwa wako, kama una hitaji mkaribishe Yesu, labda unakaribia kufirisika hilo ni hitaji, labda huna mtoto, unahitaji kitu flani, mkaribisha Yesu moyoni mwako naye atakuja ndani yako.

No comments:

Post a Comment