''Badilisha Maisha yako kwa kumpokea Yesu Kristo kuwa Mwokozi wa Maisha Yako.''

Sunday, August 26, 2018

NGUVU ILIYOMO NDANI YA INJILI

Mhubiri: Muinjilisti Gilbert Clavery
Maandiko: Mathayo 28:18-20

Mathayo 28:18-20 "18 Yesu akaja kwao, akasema nao, akawaambia, Nimepewa mamlaka yote mbinguni na duniani. 19 Basi, enendeni, mkawafanye mataifa yote kuwa wanafunzi, mkiwabatiza kwa jina la Baba, na Mwana, na Roho Mtakatifu; 20 na kuwafundisha kuyashika yote niliyowaamuru ninyi; na tazama, mimi nipo pamoja nanyi siku zote, hata ukamilifu wa dahari."

Hapa ni baada ya Yesu kufufuka kabla hajapaa, kwahiyo haya ni mahusia ya mwisho kwa wanafunzi kabla hajapaa. Ni lazima utambue kuwa Yesu tunayemhubiri, anayo mamlaka yote mbinguni na duniani. Na hii kazi ya Injili ni Yeye ndio aliyetuachia, kwahiyo unapopeleka injili fahamu kuwa umebeba mamlaka yote mbinguni na duniani, ukisema lolote lililo katika mapenzi ya Mungu kwa imani litatokea.

Alituachia mamlaka hiyo kubwa sana kwasababu alijua huko tunapoenda kupeleka injili tutakutana na mamlaka nyingine, tutapambana na mamlaka ya shetani iliyofunga watu. Na kwa jinsi mamlaka tulioachiwa na Yesu ilivyo na nguvu kubwa, shetani anakuwa hawezi kutuzuia popote! Wewe kama mtu uliyeokoka tambua kuwa una mamlaka kubwa sana ndani mwako, kwahiyo itumie hiyo kuwaambia watu wengine habari njema wafunguliwe kutoka vifungo vya shetani.

Jukumu letu lipo kwenye huo mstari wa Mathayo 28:19, kwenda kuwafanya mataifa yote kuwa wanafunzi wa Kristo. Je kama wewe umeshaokoka ni kwa kiasi gani umeshawafaya watu wengine kuwa wanafunzi wa Kristo? Unaweza kwenda kupeleka injili kwa njia nyingi; kuna ya kwenda mwenyewe kushuhudia/ kuhubiri na nyingine ya kuhubiri kwa pesa yako, kuwawezesha wengine kwenda kuhubiri, kwenda kufanya mikutano sehemu mbalimbali. 

Warumi 10:15 "Tena wahubirije, wasipopelekwa? Kama ilivyoandikwa, Ni mizuri kama nini miguu yao wahubirio habari ya mema!"

Unapotoa pesa yako kwa ajili ya Injili, usione kama umefanya kitu kidogo, kile ni kitu kikubwa sana na Mungu hawezi kukuacha kwasababu umewezesha agizo kuu kutendeka. Ukitoa kwa ajili ya injili Yesu hawezi kukuacha hivi hivi tu. Ndio kuna huduma nyingi lakini Injili ndio agizo kuu kwahiyo unapowekeza unapotoa sana kwenye injili, unapochangia kusababisha watu wapate habari ya Yesu, Yesu hawezi kukuacha kwenye mambo yako. Watu wakipata kusikia habari ya Yesu kwasababu ya pesa yako, Yesu lazima atafanya kitu kizuri kazini kwako na kwenye biashara yako. Nakusisitiza sana wekeza kwenye Injili kwa kadiri ya uwezo wako maana hutajuta.

No comments:

Post a Comment