''Badilisha Maisha yako kwa kumpokea Yesu Kristo kuwa Mwokozi wa Maisha Yako.''

Sunday, January 27, 2013

UJUMBE WA LEO: KUMPENDEZA MUNGU
-------------------------------------------------------------
Ujumbe wa leo umeletwa kwenu na Mch.Meshark Mhini. 
Maandiko: WAGALATIA 1:10, WAEFESO 5:8-10, WARUMI 14:16-18, 1WATHESALONIKE 4:1-8, 1YOHANA 2:15
------------------------------------------------------------------------------------  angalia mahubiri ya Mch.Mhini hapa




Kumpendeza Mungu ndio jukumu kuu la mkristo, vitu vyote vingine vinafuata baada ya kumpendeza Mungu. Hata kama mungu amekubariki na unajiona ya kuwa umefanikiwa sana kwa vitu vingi kimaisha lakini kama umeshindwa kuishi maisha ya kumpendeza Mungu ni sawa na kazi bure hayo maisha si kitu mbele za Mungu.
Mungu wetu ni mtakatifu sana na  anapendezwa na mtu mwenye utii na mnyenyekevu, kama mkristo yeyote hawezi kumtii Mungu kwa nyanja mbalimbali basi yote ayafanyayo bila Mungu yanakuwa  si kitu mbele zake sawa na bure. Unaweza kumpendeza mzazi, mwajiri wako, jirani au rafiki yako lakini unajikuta Mungu bado hujampa heshima iliyo sawa na hao unaowathamini, sasa swali linakuja kwetu,

Je MAISHA YAKO UNAYOISHI UNAMPENDEZA MUNGU?

Ndiyo maana tunaona mfano kwa mtume Paulo akiwauliza wagalatia je natakiwa kumpendeza mtu yeyote? Mungu anapendezwa na wale wampendao na watakatifu wasiofanya dhambi, kuna watu wengine wanaweza kutoa sadaka nzuri sana kanisani lakini jana yake ametoka kufanya dhambi, hiyo sadaka uliyotoa  Mungu hawezi ipokea, jichunguze, je unatoa fungu la kumi?, unahudhuria ibada?, unasoma neno?, unaomba? 

Hata ukiwa ofisini au kazini je unampendeza Mungu? Au ni kwa kiwango gani cha ubora ambacho hata Mungu anakikubali tumekuwa tukimpendaza Mungu? Kama tumeshindwa tu kushiriki katika shughuli mbalimbali za kikanisa kama kushiriki kwenye maombi,ibada na  idara mbalimbali kama mshirika kama za vijana ,wababa,wamama au kwaya? Je hiyo tabia inampendeza Mungu? 

Kwa kuwa umekuwa kwenye mihangaiko yako tu kila siku bila hata kumpa Mungu angalau masaa machache ili nae aweze kukutathmini na kukupa baraka au hata kumshukuru tu kwa yale aliyokufanyia wiki nzima, ndugu yangu mpendwa hebu fikiri kwa umakini je ni mangapi yenye uzuri yanatoka kwako ni lini Mungu atajivunia kitu kutoka kwako? Unarudia dhambi zilezile kila wakati na unatubu na kurudia tena na tena, je hiyo inampendeza Mungu? Hebu fikiri hilo kweli unahitaji kutubu na Mungu Wetu ni wa rehema sana huwasamehe wale wote wanyenyekeao na kutubukupondeka moyo ili waweze kumzalia Mungu matunda na kumpendeza. 

Maandiko yote yaliyopo hapo juu yamewekwa ili kukumbusha mambo mbalimbali yaliotokea huko nyuma kama mfano ili kukusaidia kuishi maisha ya utakatifu na kumpendeza Mungu. Mungu wetu ni wa upendo sana hapendi hata mmoja apotee.

Mwisho Napenda kuwatia moyo wakristo wenzangu tujitoe kikamilifu kabisa katika kumpendeza Mungu, tusiipende dunia wala mambo yote yaliyomo ndani yake, maana mtu akiipenda dunia kumpenda Mungu hakumo ndani yake.

Nawatakia  jumapili njema, na wiki yenye mafanikio, AMEN.






No comments:

Post a Comment