''Badilisha Maisha yako kwa kumpokea Yesu Kristo kuwa Mwokozi wa Maisha Yako.''

Sunday, May 19, 2019

KWANINI YESU ALIKUWA NA BIDII KATIKA KUOMBA

Mhubiri: Mch. Mussa Elias
Maandiko: Marko 1:35-39

Yesu aliamka asubuhi na mapema akaenda sehemu ya faragha KUOMBA. Yesu alikuwa analala sehemu moja na wanafunzi wake kwahiyo wanafunzi walijua alivyoondoka asubuhi na mapema kwenda kuomba. Baadae watu wa pale walikuja kumtafuta ili awahudumie kwahiyo wanafunzi wakamtafuta alipoenda kuomba, wakamwambia watu wanakuhitaji; lakini hapa cha kushangaza, akawaambia twendeni mji mwingine hakutaka tena kuwahudumia watu wa mji ule bali wa mji mwingine, hapa inamaanisha baada ya yale maombi alikuwa ashapata maelekezo ya siku hiyo kutoka kwa Baba yake, hakufanya kama anavyotaka Yeye au mazingira yalivyotaka Bali kama Baba yake anavyotaka. 

Yesu alipenda sana kutenga muda wake mzuri wa kuomba, Yeye alikuwa Mungu asilimia 100% lakini bado aliona kuna umuhimu sana wa kuomba, alipenda kujitenga na kwenda kuomba wakati wa usiku au asubuhi, hapa si maombi ya wote bali maombi binafsi. Je wewe umetenga muda mzuri wa kufanya maombi yako binafsi? Au mpaka maombi ya pamoja kanisani?

Sababu za Yesu kuwa na Bidii katika MAOMBI

1. Yesu alikuwa na mpango maalumu wa kazi ya Mungu (divine plan), alikuwa na 'plan' ndio maana alikuwa anaomba. Ili mipango yako iende vizuri ni lazima uwe na muda wa kuiombea, Yesu alikuwa na kazi mbele yake akaona kuna umuhimu wa kuiombea kwa bidii. Kama mtu una vision/ maono kwa ajili ya kazi ya Mungu ni lazima tu uombe, hapa tunaongolea maombi binafsi. Hapa Yesu alikuwa anafanya maombi binafsi sio ya wote, kama una malengo utakuwa una ratiba yako mwenyew ya kuomba sio mpaka mchungaji atangaze maombi bali lile lengo ndani yako litakuongoza kufanya maombi, Yesu lile lengo ndani yake ndio lilikuwa linamsukuma kuomba akamka asubuhi kuomba mwenyewe. 

- Ukiona huna hamu ya kuomba ujue huna lengo au maono ndani yako.

2. Alikuwa anataka muongozo wa kila siku kutoka kwa Baba yake wa mbinguni. Kutaka muongozo wa kila siku ili ufanye mambo ambayo ni mapenzi ya Mungu uyafanye katika siku hiyo. Ukiongozwa na Mungu kila siku utajua kwa uhakika nini cha kufanya na utafanya vitu sahihi kwa usahihi, sasa unaweza kupata muongozo sahihi katika siku yako kwa kuomba. 

3. Yesu hakutaka kufanya huduma yake kama mambo ya kawaida, bali kwendana na atakavyoongozwa siku hiyo, 'God is not static, God is dynamic, He gives us fresh ideas everyday'. Mungu ana uwezo wa kukupa mawazo mapya kila siku, mawazo mapya ya kufanya kazi zako, ya kufanya biashara zako. Yesu hakutaka kufanya kazi zake kama kawaida, hutakiwi umkariri Mungu bali uwe tayari kufanya anachokuagiza kwa wakati muafaka(flexible).

4. Yesu alitaka kuhudumu kwa usahihi, kwa watu sahihi na sehemu sahihi. Yesu hakuwa anahubiri hubiri tu bali alikuwa ana mpango kamili sasa huwez kufanya hivyo kama huombi. Ili kufanya kitu sahihi na kwa wakati sahihi ni lazima uwe na uongozi wa Mungu atakaye kuelekeza nini cha kufanya na lini.

5. Yesu alikuwa anataka kutekeleza tu atakayoongoza na Baba yake pekee na sio mambo mengine, hata wewe kwenye maisha yako unatakiwa ufanye yale TU unayoongozwa na Roho Mtakatifu na sio vinginevyo. Sasa huwezi kuwa hivyo kama huombi.

6. Kwa Yesu maombi yalikuwa ndio silaha pekee ya kusambaratisha kazi ya shetani, aliweza kufanya kazi kubwa ya kuondoa mapepo na kuponya watu kwasababu alikuwa anaomba vya kutosha, alikuwa anatumia muda mwingi kuomba ndio maana akienda kwenye huduma mapepo na magonjwa yanakimbia. Sasa huwezi kupata upako ule kama huombi, nguvu ile ilikuwa inatengezwa katika maombi.

Kuwa mkristo mwenye nguvu za Mungu hakuji kirahisi tu inakupasa kujitoa mwenyewe kwenye Kusoma Neno na Maombi, kuwa na muda mzuri wa maombi na sio maombi mengi ya juu juu bali maombi ya uhakika.

No comments:

Post a Comment